Watanzania waitikisa Marekani kwa utapeli


Taarifa ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Jimbo la Maryland inawataja watuhumiwa wengine katika kesi hiyo mpya kuwa ni Tibakweitira na mkewe Flavia Makundi (41), Mkazi wa Gambrills, Maryland, Carmen Johnson (46), Mwihava na Annika Boas (36) ambaye anaishi Mount Ranier, Maryland. 
KWA UFUPI
Baada ya kukiri makosa yake, hukumu ya Tibakweitira itatolewa Novemba 3 mwaka huu Saa 04:00 asubuhi, na kwa mujibu wa sheria za Maryland, adhabu ya makosa yake ni kifungo kisichozidi miaka 30 jela na faini ya Dola za Marekani milioni moja (Sh1.66 bilioni).

Washington DC. Baadhi ya Watanzania wanaoishi Marekani huenda wakaozea jela baada ya kutiwa hatiani na wengine kukiri mahakamani kuhusika katika utapeli na wizi wa mamilioni ya Dola za Marekani, kupitia mikopo na upangishaji wa nyumba.
Hukumu ya hivi karibuni ni ya Mtanzania, Mokorya Cosmas Wambura (41) ambaye alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela na faini zaidi ya Dola 400,000 (zaidi ya Sh660 milioni) baada ya kutiwa hatiani kwa makosa ya kutumia vitambulisho vya wizi na taarifa za kibenki za kughushi kufanya udanganyifu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Maryland, Deborah Chasanow katika hukumu yake, pia alisema Wambura ataendelea kuwa chini ya uangalizi kwa miaka mitano baada ya kumaliza kutumikia kifungo jela.
Wambura ambaye ni mkazi wa Takoma Park, Maryland alitiwa hatiani kwa kula njama za wizi wa mtandao na kuhusika katika matukio mawili tofauti ya kujipatia fedha kwa udanganyifu, akitumia vitambulisho vya wizi.
Hukumu dhidi ya Wambura imetolewa wakati ambao Watanzania wengine kadhaa wakiwamo wawili waliokuwa washirika wake wakisubiri hukumu zao, baada ya kukiri kufanya makosa ya utapeli, kujipatia fedha kwa udanganyifu na wizi wa kutumia mtandao.
Watanzania hao ni Edgar Tibakweitira, ambaye pia anajulikana kwa majina mengine; Edgar Julian, Charles Edgar Tibakweitira na Edgar Gaudious Tibakweitira ambaye licha ya kukiri makosa yake pia alikubali kutoa gari lake aina ya Range Rover, kama sehemu ya malipo ya fedha atakazoamriwa kulipa na mahakama.
Baada ya kukiri makosa yake, hukumu ya Tibakweitira itatolewa Novemba 3 mwaka huu Saa 04:00 asubuhi, na kwa mujibu wa sheria za Maryland, adhabu ya makosa yake ni kifungo kisichozidi miaka 30 jela na faini ya Dola za Marekani milioni moja (Sh1.66 bilioni).
Mbali na Tibakweitira ambaye ni mkazi wa Severn, Maryland, Mtanzania mwingine ambaye pia alikuwa mshirika wa Wambura ni Mrisho Mavuruma Mzese ambaye alitiwa hatiani Mei 1, 2014 kwa makosa 11 yanayohusiana na utapeli na wizi kwa njia ya mtandao.
Hukumu dhidi ya Mzese imepangwa kutolewa Agosti 7 mwaka huu Saa 8:00 mchana, huku akikabiliwa na adhabu kama ya Tibakweitira kwa mujibu wa sheria za Maryland.
Aprili 22 mwaka huu, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Jimbo la Maryland ilitoa taarifa kuhusu Watanzania wengine wawili ambao walikiri mahakamani makosa ya kujipatia fedha kwa udanganyifu baada ya kutoa taarifa za uongo kuhusu ununuzi wa nyumba na ukarabati wa nyumba hizo.
Watanzania hao ni mkazi wa Ashburn, Virginia, Nsane Phanuel Ligate (42) ambaye ni wakala wa uuzaji wa nyumba na mshirika wake wa karibu Cane Mwihava (43) mkazi wa Bowie, Maryland.
Watuhumiwa hao wanakabiliwa na adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela na kulipa faini ya Dola za Marekani milioni moja (Sh1.66 bilioni), watakapohukumiwa na Jaji Chasanow. Hukumu dhidi ya Mwihava imepangwa kutolewa Oktoba 14 mwaka huu saa 7:00 mchana wakati Ligate amepangwa kuhukumiwa siku mbili baadaye, Oktoba 16, 2014 saa 4:00 asubuhi.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ujerumani yanyakua Kombe la nne la Dunia

Abu Bakr al-Baghdadi: Nguo ya ndani ya kiongozi wa IS 'iliibiwa' kufanya uchunguzi wa DNA

HILI NDILO BIFU KUBWA KATI YA RIHANA NA NICK MINAJ.