Ridhiwani ataja 11 wanaotosha kugombea urais 2015


Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete akizungumza wakati wa mahojiano maalumu na Mhariri Mtendaji wa gazeti la Mwananchi, Frank Sanga, mjini Dodoma hivi karibuni. Picha na Edwin Mjwahuzi      

KWA UFUPI
Ridhiwani (35), ambaye alishinda kiti cha ubunge wa Jimbo la Chalinze Aprili mwaka huu, alitaja majina hayo katika mahojiano maalumu na gazeti hili yaliyofanyika mjini Dodoma hivi karibuni.

Dar es Salaam. Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete ametaja majina 11 ya wanachama wa CCM wanaofaa kuwania urais kurithi kiti cha baba yake, Rais Jakaya Kikwete anayemaliza muda wake mwakani.
Ridhiwani (35), ambaye alishinda kiti cha ubunge wa Jimbo la Chalinze Aprili mwaka huu, alitaja majina hayo katika mahojiano maalumu na gazeti hili yaliyofanyika mjini Dodoma hivi karibuni.
Miongoni mwa aliowataja kuwa wana sifa ni makada watano walio chini ya uangalizi wa CCM wa mwaka mmoja baada ya kubainika kuanza kampeni za urais mapema, mawaziri wawili waliopoteza nyadhifa zao katika kashfa ya Operesheni Tokomeza, mwanamke mmoja na Rais wa Zanzibar.
“Kutaja majina tu, naweza kuorodhesha wengi tu. Naweza kuorodhesha hata watu 500, kwa sababu tunaona wengi sana,” alisema mtoto huyo wa Rais Kikwete ambaye amekuwa ndani ya CCM kwa muda mrefu akitokea umoja wa vijana wa chama hicho, UVCCM. “Kwa mfano, kwa upande wa Bara tunao Emmanuel Nchimbi, William Ngeleja, January Makamba, Bernard Membe, Steven Wassira, Edward Lowassa na Asha-Rose Migiro,” alisema.
Aliongeza: “Hawa ni kwa uchache zaidi… ni baadhi ya watu ambao wanatajwa kwa upande wa Bara, lakini jambo la msingi ni nani mwenye sifa za kuwa rais.”
Alisema pamoja na kwamba wanasiasa hao wote wanazo sifa za kuiwania nafasi hiyo ya juu, vikao vya chama ndivyo vitakuwa na nafasi ya kuwachuja ili kupata wanaotosha. “Kama wanatosha au la, vikao vya chama vitakaa kuamua licha ya kuwa hao wote niliowataja, kwa sifa za kugombea urais wote wanajitosheleza. Wana sifa, wana uwezo wa kugombea na wana uwezo wa kushinda, hao ni kwa upande wa Bara,” alisema.
Alipoulizwa hali ikoje kwa upande wa Zanzibar, Ridhiwani alisema, “Sisi chama chetu kina utajiri wa watu kwa upande wa Zanzibar kuna Shamsi Vuai Nahodha, Hussein Ali Mwinyi, Dk Seif Ally Iddi (Makamu wa pili wa Rais Zanzibar) na Dk Mohammed Ali Shein, Rais wa Zanzibar. Hawa ni watu ambao wana uwezo na hata wakipewa jukumu la kuongoza nchi hii wanaweza. Tunao wengi sana.”
Membe, Wassira, Lowassa, Ngeleja na Makamba walipewa adhabu na Kamati ya Maadili ya CCM ya kutogombea nafasi yoyote ndani ya chama wala kufanya kampeni baada ya kudaiwa kukiuka taratibu za chama hicho, wakati Nchimbi na Nahodha walilazimika kujiuzulu nyadhifa zao za uwaziri kutokana na kashfa ya Operesheni Tokomeza ambayo ililenga kushughulikia majangili, lakini ikahusishwa na vitendo vya ukiukaji haki za binadamu.
Ridhiwani hakumtaja Waziri Mkuu wa zamani, Fredrick Sumaye ambaye pia anatumikia adhabu hiyo ya Kamati ya Maadili ya CCM.
Baadhi kukwama
Hata hivyo, Ridhiwani alidokeza kuwa wapo baadhi ya wanasiasa watakaokwama kufikia lengo hilo kutokana na kukabiliwa na kesi ndani ya chama, ambazo hakuzitaja wala kutaja wahusika.
“Kuna watakaopungua kutokana na kesi zinazowakabili katika chama ambazo zinawafanya wapungukiwe sifa. Kwa maana hiyo kuna watu kama wanne hivi (wa Bara) unawatoa na ukiwatoa unabakiwa na watatu, sasa unaweza kujiuliza hao watakaobaki watatu, je, wanatosha?”

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ujerumani yanyakua Kombe la nne la Dunia

Abu Bakr al-Baghdadi: Nguo ya ndani ya kiongozi wa IS 'iliibiwa' kufanya uchunguzi wa DNA

HILI NDILO BIFU KUBWA KATI YA RIHANA NA NICK MINAJ.