JIWE Laporomoka jijini Mwanza na kuua Watu Wanne


Vilio na simanzi jana vilitawala kwa wakazi wa maeneo ya Sinai-Mabatini, baada ya vifo vya watu wanne wa familia mbili tofauti, vilivyotokana na mvua iliyosababisha miamba mikubwa ya mawe kuporomoka na kuponda nyumba zao usiku wa manane. 
 
Tukio hilo la kusikitisha limeripotiwa kutokea saa nane usiku kuamkia jana, wakati mvua   iliyoambatana na upepo wa wastani ilipokuwa ikiendelea kunyesha, na kusababisha miamba hiyo mikubwa inayokadiriwa kufikia tani mbili kuporomoka na kuziponda nyumba hizo na kusababisha vifo hivyo na majeruhi wanne. 
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Valentino Mlowola, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuwataka wananchi kuchukua tahadhari wakati wa mvua.
 
Mpekuzi ilifanikiwa kufika eneo la tukio na kushuhudia miamba hiyo ikiwa imeharibu nyumba, huku nyumba moja iliyojengwa kwa matofali ya tope ikiwa imeanguka na kubaki kifusi.
 
Nyumba zilizokumbwa na maafa hayo zinamilikiwa na watu waliotajwa kwa majina ya Joseph William na Lameck Ajiji, na kila moja watu wawili wamefariki kwa kukandamizwa na miamba hiyo.
jiwe1
 
Katika nyumba ya William iliyokuwa na watu watano, waliofariki wametajwa kuwa ni Kefa Joseph (15) na Emmanuel Joseph (12), wote wanafunzi wa Shule ya Msingi Mbugani na majeruhi mmoja ambaye hakufahamika jina lake ambaye alikimbizwa hospitali.
 
Nyumba inayomilikiwa na Ajiji yenye watu watatu, waliofariki wametambuliwa kuwa ni mama wa nyumba hiyo, Kwinta Geko (24) na mumewe Samson Odinya.
 
Waliojeruhiwa ni mtoto Bety Samson (4) na Godfrey Joseph (14) mwanafunzi wa Shule ya Msingi Mbugani.
 
Tukio hilo ni la pili kutokea katika eneo hilo la Sinai. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka 2009 baada ya miamba kuporomoka na kusababisha vifo vya watu wawili wa familia moja.
 
Tukio la jana lilivuta hisia tofauti kwa wakazi wa Jiji la Mwanza, huku wengine wakiangua vilio.jiwe2
Mamia ya wananchi waliofika eneo hilo, walijitolea kwa kumpa fedha mtoto Bety aliyenusurika kufa kutokana na tukio hilo.
 
Mbunge wa Nyamagana jijini Mwanza, Ezekiel Wenje (Chadema), alifika eneo la tukio na kutoa pole kwa wananchi, ndugu jamaa na marafiki wa familia zilizoathirika na janga hilo, ambapo alionyesha kushtuka baada ya kuelezwa na wananchi kwamba hakuna kiongozi yeyote wa Serikali aliyefika eneo hilo.
 
Akizungumza kwa kutumia kipaza sauti mbele ya umati wa watu waliokuwa wamefurika katika eneo hilo la tukio, alisema: “Inashangaza sana kuona hata mkuu wa wilaya hajafika hapa. Nitawasiliana na viongozi wa Serikali na mchana nitarudi hapa tena.”
 
Baadhi ya wananchi waliozungumza na Mwandishi katika eneo la tukio, waliiomba Serikali kuzuia wananchi kujenga karibu na miamba mikubwa, kwani kufanya hivyo itasaidia sana kuepusha maafa kama hayo.
 
“Kwa kweli tukio hili linasikitisha sana, na tunaomba viongozi wa serikali wasaidie wananchi kuwaondosha kwenye maeneo ya kwenye miamba,” alisema mmoja wa wananchi hao ambaye pia ni balozi wa Shina Namba Tano, Mtaa wa Nyerere A, Jackson Kitundu.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ujerumani yanyakua Kombe la nne la Dunia

Abu Bakr al-Baghdadi: Nguo ya ndani ya kiongozi wa IS 'iliibiwa' kufanya uchunguzi wa DNA

HILI NDILO BIFU KUBWA KATI YA RIHANA NA NICK MINAJ.