VITAMBULISHO VYA KURA VYAFUTWA, KUTOLEWA UPYA!

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Mstaafu Damian Lubuva akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari Dar es Salaam jana. Kulia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume hiyo Julius Mallaba. PICHA | JOSEPH ZABLON 
KWA UFUPI
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imetangaza matumizi ya teknolojia mpya ya Biometric Voter Registration (BVR), katika maboresho ya Daftari la Kudumu la Wapigakura ambayo yatafuta matumizi ya vitambulisho vya kupigia kura vya sasa.

Dar es Salaam. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imetangaza matumizi ya teknolojia mpya ya Biometric Voter Registration (BVR), katika maboresho ya Daftari la Kudumu la Wapigakura ambayo yatafuta matumizi ya vitambulisho vya kupigia kura vya sasa.
Kwa hatua hiyo, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva ametangaza kuwa: “Katika kura ya maoni ya Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu wa 2015, mpigakura atatumia kitambulisho kipya atakachopatiwa na Tume baada ya kuandikishwa upya katika mfumo huu na si vinginevyo.
Vitambulisho vilivyotolewa katika uandikishaji na uboreshaji uliopita havitatumika tena.”
Akitangaza mpango huo mpya Dar es Salaam jana, Jaji Lubuva alisema Tume hiyo itaanza maboresho ya daftari hilo kwa watu wote wenye sifa za kupiga kura Septemba mwaka huu na kukamilisha kabla ya kura ya maoni ya Katiba na Uchaguzi Mkuu 2015.
BVR ni mfumo wa kuchukua taarifa za mtu za kibaiolojia hasa alama za vidole.
Mwaka 2004, NEC ilianzisha Daftari la Kudumu la Wapigakura ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa taarifa za wapigakura na uhifadhi wa taarifa za kielektroniki.
Sanjari na hilo, tume hiyo ilitoa vitambulisho vya wapigakura ambavyo pia vimekuwa vikitumika kwa shughuli mbalimbali za utambulisho katika maeneo kama benki, polisi, mahakamani, uhamiaji, ukataji leseni, usajili wa simu na mengineyo.
Jaji Lubuva alisema katika kazi hiyo ya uandikishaji, NEC imekusudia kutumia Sh293 bilioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa, mafunzo ya watendaji na uandikishaji.
Maofisa watakaotumika katika uandikishaji ni pamoja na waratibu wa uandikishaji wa mkoa, maofisa waandikishaji ambao watakuwa ni wakurugenzi wa halmashauri, maofisa wasaidizi watakaokuwa watatu kwa kila jimbo, watendaji kata na waratibu wa elimu.
Mafunzo kwa watendaji hao yanatarajiwa kuanza Julai, 2014 na uandikishaji utaanza Septemba na katika vituo 40,015 kote nchini.
Vituo vya uandikishaji
Jaji Lubuva alisema kwa utaratibu wa sasa, vituo vya kujiandikishia vimeongezeka kutoka 24,919 hadi 40,015 ambavyo vimewekwa katika ngazi za vitongoji, vijiji na mitaa ili kuwezesha kuwa karibu zaidi na wananchi.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ujerumani yanyakua Kombe la nne la Dunia

Abu Bakr al-Baghdadi: Nguo ya ndani ya kiongozi wa IS 'iliibiwa' kufanya uchunguzi wa DNA

HILI NDILO BIFU KUBWA KATI YA RIHANA NA NICK MINAJ.